PACSO YATETA NA WANANCHI KOJANI
MTANDAO wa Asasi za kiraia wa Pemba (PACSO) umeandaa mkutano maalumu kwa wananchi wa Kisiwa kidogo cha Kojani wenye lengo la kuiwezesha jamii kupata uwelewa mpana juu ya masuala ya kisheria na haki za binaadamu. Mkutano huo uliowashirikisha wananchi wa Kisiwa cha Kojani umeandaliwa na jumuiya PACSO kwa ufadhili wa shirika la UNDP na kufanyika huko ukumbi wa skuli ya msingi Kisiwani humo. Akizungumza na wananchi Mkurugenzi Mkuu wa PACSO Pemba Mohamed Najim Omar katika mkutano huo alisema, mpango huo una lengo la kuiwezesha jamii kupata ufahamu wa kisheria na haki za binaadamu. "Jamii zetu bado zina changamoto nyingi na baada ya kuliona hili tumeamua kuandaa mpango wa kupita kwenye jamii kutoa taaluma ya kuwawezesha watu ufahamu juu mambo haya, elimu zinatolewa nyingi lakini na sisi pia tumeona kuja haja ya kuwafikia", alisema. Aidha alisema, kutokana na kujitokeza masuala mbali mbali ya unyanyasaji wa kijinsia, watoto kudhalilishwa, wanawake, watu wenye ulemavu na hata wazee ...