KUVUNJIKA KWA NDOA NA HATARI ZA WATOTO WA

 

KIKE KUKATISHA NDOTO ZAO

 

Na HABIBA ZARALI PEMBA

NDOTO za watoto wengi wa kike huanza kujengwa tangu wakiwa wadogo.

Wengine hutamani kuwa madaktari, walimu, wanasheria au wataalamu watakaosaidia familia zao na taifa kwa ujumla.

Hata hivyo, kwa baadhi ya watoto wa kike, ndoto hizo zimekuwa zikififia na hatimaye kutoweka kutokana na changamoto zinazotokana na kuvunjika kwa ndoa za wazazi wao.

Ingawa talaka huonekana kuwa mwisho wa uhusiano wa wanandoa, ukweli ni kwamba athari zake huendelea kuonekana kwa muda mrefu katika maisha ya watoto.

Watoto wa kike ndio huonekana kubeba mzigo mkubwa zaidi, wakikabiliwa na hatari ya kuacha shule, kuozeshwa mapema, kukosa malezi bora au kushindwa kufikia ndoto walizojijengea tangu utotoni.

Katika Mkoa wa Kaskazini Pemba Wilaya ya Micheweni na maeneo mengine, simulizi za watoto wa kike walioathirika zinaonesha namna migogoro ya kifamilia inavyoweza kubadili kabisa mwelekeo wa maisha yao.

Pamoja na Hali hiyo kuwepo lakini inaonekana kujificha na kuumiza polepole bila ya kujulikana kiurahisi huku maumivu na athari ya watoto wa kike ikiendelea.

Fatma Ali Juma (16) wa Micheweni alikuwa na ndoto ya kuwa daktari, tangu akiwa mdogo alipenda masomo ya sayansi na aliamini siku moja angevaa koti jeupe na kuwahudumia wagonjwa hospitalini.

 

 

 

Hata hivyo, baada ya wazazi wake kuachana, hali ya maisha ilibadilika, changamoto za malezi na ukosefu wa mazingira mazuri ya kuendelea na masomo zilianza kujitokeza na kuathiri safari yake ya elimu.

Ndoto yake ya kuwa daktari ikaanza kufifia taratibu na kujiona kabakia tu bila muelekeo wowote  ule kwani hakuna mzazi yoyote aliemshughulikia maendeleo yake ya elimu na badala yake ilikuwa ni uhasama dhidi yao.

“Mimi licha ya hamu kubwa niliyokuwa nayo ya kusoma hadi kufikia udaktari ilikufa baada ya wazazi wangu kuachana alisema kwa huzuni.

Shufaa Said Faki wa Micheweni, ndoto yake ilikuwa ni kuwa mwalimu, alitamani kusimama mbele ya darasa na kuwafundisha watoto ili kuwasaidia kufikia mafanikio yao.

Lakini baada ya wazazi wake kuachana na kukosekana kwa mawasiliano mazuri kati yao, maisha yake yalibadilika,Katika mazingira hayo, Shufaa aliozeshwa akiwa bado mdogo kabla hajamaliza masomo yake.

“Ndoa yangu ya mapema ilikatiza safari yangu ya elimu na kuzima ndoto nilikuwa nayo ya kuwa niwe mwalimu”, alisema.

Katika kijiji cha Msuka Wilaya ya Michweni, Aziza Bakar alikuwa na ndoto ya kuwa mwanasheria, alitamani kutetea haki za watu na kusaidia jamii kupitia taaluma ya sheria.

Leo hii anaamini kuwa kama angepata mazingira bora ya malezi na msaada wa kutosha, angekuwa karibu zaidi na kutimiza ndoto yake.

“Baada ya wazazi wangu kuachana nililelewa na bibi nikawa sina hata msukumo wa kusoma” alieleza.

Naye Maryam Ali Zahor wa Gando Wilaya ya Wete alikuwa na ndoto ya kufanya kazi ofisini na kujitegemea kupitia elimu yake.

Aliona elimu kama daraja la kufikia maisha bora ingawa changamoto za kifamilia zilizotokana na kuvunjika kwa ndoa ya wazazi wake, ziliathiri safari ya masomo na matumaini yake ya kufikia malengo,

Afisa ustawi wa jamii Wilaya ya Wete Mkoa wa Kaskazini Pemba Salama Saleh Hamad anataja kesi 34 zikiwemo 16 za huduma na 18 za mvutano wa malezi zimeripotiwa kwa mwezi January hadi Aprili 2026.

 

 

 

Kesi za migogoro ya ndoa zilizoripotiwa zilikuwa ni tano ambapo madai ya talaka zilikuwa mbili.

Anasema athari kwa watoto wa kike ni kukosa huduma muhimu ikiwemo elimu na kuathiri msongo wa mawazo na kubakia kudhalilika .

Mzazi Asha Suheil wa Chimba ,anakiri talaka zimekuwa miongoni mwa sababu zinazowakwamisha watoto wa kike kutimiza ndoto zao.

 

“Baadhi ya akina baba huondoka kwa muda mrefu kwenda nje ya maeneo yao ya makazi, huacha familia bila huduma muhimu na wakati mwingine huwapa talaka wake zao bila sababu za msingi.

“Matokeo yake wazazi wanapogombana na kutengana watoto ndio wanaobeba maumivu na athari kubwa zaidi, anasema.

Naye Moza Faki Shaaban wa Finya anasema migogoro ya kifamilia mara nyingi husababisha mahitaji muhimu ya watoto kuwekwa pembeni.“Wakati wazazi wanapokuwa katika mgogoro, suala la elimu, afya na mahitaji mengine ya watoto hupoteza kipaumbele mwishowe watoto ndio wanaoumia zaidi, anasema.

Faki Abdalla Shauri wa Konde anasema anajutia kitendo alichokifanya cha kumuacha mke aliyezaa nae watoto nane, huku akisisitiza wanandoa kuwa na busara bila hivyo ndoa huvunjika na kusambaratisha watoto.

Fatma Shaaban Omar wa Wete ni mmoja  kati ya wanawake walioachwa akiwa na watoto sita, anasema ugumu wa maisha ,ulezi wa watoto hao sita pekee bila usaidizi wa baba kunapelekea kukosa huduma muhimu ikiwemo chakula, elimu ,mavazi.

 

“Wanawake tunatwishwa mzigo mzito kwani wanaume wanapotuacha na tukiwa tayari tumeshazaa watoto ndio wanaohangaika”anasema.

Nae Sada Ali Juma wa Konde ambae ameachwa na watoto wanne wote wakiwa wanawake  anasema kutokana na ulezi wa peke yake imebidi watoto wake wajishughulishe na ajira za utotoni ikiwemo kuuza biashara ndogondogo, ili wapate mahitaji hasa ya chakula.

Kutokana na hali hiyo, Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA Zanzibar) kinatekeleza mradi wa tunaweza pamoja kumaliza udhalilishaji wakijinsia kwa wanawake na wasichana EVAWG.

 

Mradi huo ambao kwa kisiwa cha Pemba umejikita Mkoa wa kaskazini utaweza kuibua changamoto zilizojificha ambazo zinawarejesha nyuma wasichana na watoto wakike na kudhalilishwa.

Mratibu wa mradi huo Asya Hakim Makame anasema tathmini zilizofanywa na shirika hilo zimeonesha kuwa

watoto wengi wanaokulia katika malezi ya upande mmoja hukabiliwa na changamoto za elimu, malezi na ustawi wa kisaikolojia.

“Tulibaini kuwa talaka ni miongoni mwa sababu zinazochangia ongezeko la watoto wanaolelewa na mzazi mmoja.

“Watoto wa kike ndio wanaoathirika zaidi kwa kuwa baadhi yao hulazimika kuacha skuli, kuingia katika ndoa za mapema au kukosa msaada unaohitajika kufikia ndoto zao”, anasema.

Kwa mujibu wa TAMWA, mradi huo unalenga kuongeza uelewa kwa wazazi, viongozi wa dini, viongozi wa serikali na jamii kwa ujumla kuhusu umuhimu wa kulinda haki za mtoto na kuhakikisha kuwa migogoro ya wazazi haiwi sababu ya kuwanyima watoto fursa za maendeleo.

Mwalimu wa skuli ya Sekondari ya Msuka Wilaya ya Micheweni Amini Khamis Khatib anasema mara nyingi wanafunzi hasa wa kike wanapotoka katika familia zenye migogoro huonesha kushuka kwa mahudhurio, ufaulu na kujiamini.

“Wanafunzi hao wapo hasa wa kike ingawa tunapowagunduwa tunawapa ushauri mzuri kuwaondowa na msongo wa mawazo ili waweze kusoma huku wakitimiza malengo yao”,anasema.

Mshauri nasaha Fatma Mohamed Khalfan anasema wazazi wanapoachana kuna maumivu ya kihisia anayapata mtoto, na kujawa na huzuni huku  akijiona duni na hana thamani.

Anasema talaka inaathiri jamii kwa kuongezeka watoto wa mitaani wanaoweza kujishughulisha na vikundi viovu na hatimae kuwa wizi ama watumiaji madawa ya kulevya.

Kwa mujibu wa sensa ya watu na makaazi ya 2022 , ripoti ya OECD inayotumia takwimu za Tanzania inaonesha

kuwa asilimia 37 ya wanawake wenye umri wa miaka 15 na zaidi Kaskazini Pemba waliopewa kabla ya kutimiza miaka 18.

Ambapo kwa mujibu wa sensa hiohio Mkoa wa Kaskazini Pemba una asilimia 17.5 walioacha skuli.

Akizungumzia suala hilo, Sheikh  Said Abdalla kutoka ofisi ya mufti Pemba anasema uislamu unatambua talaka kama suluhisho la mwisho pale maridhiano yanaposhindikana, lakini hauondoi wajibu wa wazazi kwawatoto wao.

“Katika Uislamu, mtoto ana haki ya kupata malezi, elimu, matunzo na mapenzi kutoka kwa wazazi wake, talaka inaweza kuvunja ndoa, lakini haiwezi kuvunja wajibu wa wazazi kwa watoto wao”, anasema.

 

 

 

Mchungaji wa Kanisa la ‘TAG’ Kaskazini Pemba Samwel Elias Maganga anasema familia ni taasisi ya kwanza ya malezi iliyowekwa na Mungu na kwamba wazazi wanapaswa kuhakikisha watoto hawawi waathirika wa migogoro yao.

 

 

 


“Watoto wanahitaji upendo, mwongozo na usalama wa

 

kihisia, migogoro ya ndoa isipopewa ufumbuzi mzuri,

 

watoto ndio hubeba maumivu yake kwa muda mrefu

 

zaidi, anasema.

 

 

 

Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Pemba, Mgeni Khatib Yahya, anasema serikali inaendelea kuweka mazingira bora ya kuhakikisha watoto wote, hususan watoto wa kike, wanapata haki zao za msingi ikiwemo elimu, malezi bora na ulinzi dhidi ya changamoto z

Comments

Popular posts from this blog

UMUHIMU WA VITUO VYA TUTU KWA MAKUZI YA MTOTO

UHABA WA VITUO VYA POLISI WILAYA YA CHAKE CHAKE BADO MLIMA MREFU KUDHIBITI UHALIFU VITENDO VYA UDHALILISHAJI NA UVUNJIFU WA HAKI ZA BINAADAMU.

PACSO YATETA NA WANANCHI KOJANI