UHABA WA VITUO VYA POLISI WILAYA YA CHAKE CHAKE BADO MLIMA MREFU KUDHIBITI UHALIFU VITENDO VYA UDHALILISHAJI NA UVUNJIFU WA HAKI ZA BINAADAMU.






NA  AMINA AHMED MOH’D - PEMBA 

CHAKE Chake ni moja kati ya  wilaya mbilizi zinazopatikana katika  Mkoa wa Kusini Pemba  Zanzibar Tanzania. 
Ambayo kwa mujibu wa sensa ya  mwaka 2012  ina idadi ya wakaazi 97,249 na anuani za makazi zikiwa ni   74200  
 

Idadi Mpya  ya wakaazi wa Chake Chake   kwa takwimu za Sensa  ya watu na makazi  ya mwaka 2022 iliyotolewa hivi karibuni  bado hazijapokelewa katika ngazi za  wilaya   ni kutokana na takwimu hizo kuikiishia  katika ngazi za Mikoa pekee jambo ambalo limewia ugumu kupatikana  idadi mpya  ya wakazi wake wa sasa. 
 
 Chake Chake ina jumla ya shehia 32 ambazo wakaazi  wake hulazimika  kutumia kituo kimoja pekee  cha polisi  katika kuripoti  matukio mbali mbali. 

Matukio hayo ni pamoja uhalifu, udhalilishaji wa kijinsia wazee wanawake na watoto, wizi wa mazao , mifugo,  Pamoja na Ajali za Barabarani . 

Akina mama  na watoto hukwazika  zaidi kukifikia kituo hicho bila kujua hatima na ufumbuzi wa suala hilo utakuwa lini .

Baadhi ya  wakaazi wa chake chake wanasema   kuwa matumaini   yao ni kusogezewa kwa karibu   vituo vya polisi  katika shehia zao ili kuondokana na usumbufu. 

" Tuna matumani  na serikali pamoja   na watu wenye uwezo  kutusaidia kutuongezea vituo   vya polisi wilayani kwetu na kwa vile tukionana na viongozi  wahusika akiwemo mkuu wa wilaya  tunalalamika  sana  suala hili. 

Ni maneno ya " Pascal Mkuba  mwanaharakati  wa   dini  juu ya kupinga udhalilishaji wa kijinsia Gombani Chake Chake. 
 
" Tupo tayari kujitolea  nguvu zetu , tushike pauro tubebe mabero yaani uwezo wa kujenga hatuna lakini uwezo  kujitolea nguvu kusaidia tuko tayari ". Akaongeza pascal Mkuba  

"Kituo kimoja pekee kinarudisha nyuma mapambano dhidi ya udhalilishaji  na  Matukio mengi   huishia njiani kutokana umbali wakufata kituo kwajili ya kuripoti matukio. 

Watu hufanya suluhu  na kuishia majumbani baadhi ya kesi za udhalilishaji zinapojitokeza hawaendi vituoni wanahofia umbali lakini vingekuwa vipo karibu matukio yakitokea yanaripotiwa  tu kama sehemu nyengine. 

Saivi mtoto   wa miaka 16 kakatishwa masomo   kesi haijenda popote anaolewa siku mbili anarudishwa kwao haki yake ya kusoma kaikosa , 
Akaendelea "kwa mume hajakaa na kawa mkosaji hana pakudai haki walau akarudishwa skuli yupo tu " . 

Ni Maneno ya Saumu Ali mkaazi wa Ole . 

" Watoto  hawatuogopi tena unamkataza kitu hichi kibaya anafanya hicho hicho ukiona  kawa msugu anapelekwa polisi ijapo kutishiwa inakuwa dawa anaogopa

 Lakini ngumu tunawaacha tu mana mpka ukifunga safari  kuenda uko kituoni  si leo kesho na kesho kutwa wamekuwa wizi kwa vile wamekosa miongozo mapema. 

Tunaibiwa mifugo yetu inachinjwa  usiku   huko huko tulikoilaza  mtu ata akipiga kelele muibaji anaacha kisu  na mapolo apo apo anakimbia  

Tusubiri asubuhi tuende Kutoa tarifa polisi  mana uwezo wa kuenda kwa  miguu kutoa taarifa  hatuna  kituo mpka uende  Chake mjini    ". 

" Tunamuomba Dokta  Mwinyi  atusaidie kutuondolea usumbufu  tunaoupata sisi akina mama  mifugo  yetu inaibiwa 

Tunakosa haki zetu kutokana na kushindwa kufikia kwa wakati sahihi vituoni kutoa taarifa za kuibiwa". 

"Binafsi mwaka huu nimeibiwa Ng'ombe wangu  akachinjwa  lakini  kesi nikaenda polisi siku moja zilizobakia sijaenda kufuatilia mpka kesho. 

 Inabaki kumbukumbu tu nilichoka kwenda na kurudi kila siku Nimerudia nyuma kimaendeleo " .

Ni maneno ya bi Asha Bakari Juma mkaazi Wa Kijiji Cha  Simaongwe Shehia ya Mjini Ole wilaya ya Chake Chake.

 "Haki za binaadamu hazipo  zinakosekana kabisa kuna nyakati tumekuwa tukiogopa hata kukatisha njia na watoto 

Vurugu za vyombo vya miguu miwili nyakati za jioni na usiku  wale hawana  kofia ngumu, wale wanaendesha wanavyojua" . 

"kwa sababu hakuna polisi  imekuwa vijana  wanapoteza nguvu kazi na kupoteza maisha  huku kwetu zaidi, 

kungekuwepo na kituo hakuna kijana angeendesha chombo ovyo akapita mbele ya kituo anajua atachukuliwa hatua lakini hakuna anafanya anavyojiskia ". 

" Serikali  tunaomba itusaidie kuwekwe kituo na sehemu nyengine zenye barabara za ndani  vijana wanapoteza maisha kizembe . 

"Mkasi Haji Mkaazi wa Wesha.

Mzee Hassan Yakoub alisema kuwa  Baadhi ya vijana wasiopenda amani wamekuwa wakiutumia mwanya huo kufanya vitendo vya uhalifu .

"Tunaomba  Tusogezewe karibu vituo vya polisi Sababu  vitendo vya  uhalifu vinavunja amani   na  watu hujichukulia sheria mikononi   mwao kwa vile vyombo vya sheria  havipo karibu yao". Alidai  Mzee huyo mkaazi wa Ole

 "Mbuzini ndio shehia ambayo ina  lango kuu  la kuingilia na kutokea chake chake hapa ndio kuna umuhimu mkubwa wa kuwepo kituo cha polisi  lakini hakipo. 

kudhibiti uhalifu Tunaiomba serikali na wahisani  itusaidie  suala hili tunataka chake chake ambayo  haina uhalifu". 

Hemed Abeid Hemed Sheha wa shehia ya Mbuzini Wilaya ya Chake Chake. 

SHEHIA AMBAYO IPO KARIBU SANA NA KITUO CHA POLISI INASEMAJE. 

  
Mafunda hamad Rubea Sheha wa shehia ya Madungu anasema  Matukio  mengi ya kiuhalifu yanayoripitiwa kwake yamekuwa na urahisi kufikishwa kituoni kutokana na kuwa karibu na kituo. 


"Kesi za udhalilishaji  zinaporipotiwa  kwangu  dakika tumezifikisha kituoni ufuatiliaji unaanza zinapelekwa mahakamani  hazina nenda uje ambayo itawasumbua wananchi wangu

 Mtu anamudu kuenda kituoni hata kwa miguu ni jambo la kujivunia kuwa karibu na kituo, lakini hata uhalifu  sio mara nyingi kuskia kumeibiwa nguo mara mifugo mazao tunajivunia ilo ubalifu ni mchache ". 

Wakaazi wilaya ya Chake Chake wanazidi kuongezeka  katika maeneo ya miji na vijiji na hii inasababishwa ni kutokana na kuwepo mji mkuu wa  kibiashara  ambapo wannanchi wengi kutoka nje ya wilaya hiyo hulazimika kufuata mahitaji mengi  katika mji huo.

 Ofisi Ya Mkurugenzi wa Mashtaka  Mkoa wa kusini Pemba  mkoa ambao umeundwa kuputia wilaya mbili Mkoani na Chake Chake  inasema  inapokea  kesi nyingi zaidi za makosa na  vitendo mbali mbali  vya uhalifu h kutoka wilaya ya  Chake Kuliko wilaya ya Mkoani. 

"Wilaya ya hake tunapokea kesi nyingi zaidi kuliko Wilaya ya Mkoani na zinatokea kesi na jalada linaletwa Ofisini lakini  kutokana na ushahidi kuwa dhaifu tunaelekeza kufungwa. 

kutokana na kukosa ushahidi zipo  kesi ambazo watu walifunguwa na  kushindwa kurudi tena  kufuatilia Zipo kesi ambazo aliefanya kosa hajulikani alieripoti kaja siku moja tu harudi tena". 

"Sababu zinaweza kuwa nyingi zinazopelekea tofauti hiyo kiwilaya kwanza  Wilaya ya Chake ina idadi kubwa ya watu kuliko mkoani. 

lakini Wilaya ya chake ni wilaya yenye mji  mkubwa kuliko mkoani, na wilaya zote ambazo zina miji makosa ni mengi kuliko ambazo hazina mijini kifupi mjini makosa ni mengi na wahalifu ni wengi". 

jengine wilaya ya Chake ina upungufu wa vituo vya Polisi, kipo kimoja tu tofauti na wilaya ya Mkoani yenye vituo vitatu vya Polisi Pia inapelekea kupungua kwa makosa endapo vituo vikiwa karibu na wahalifu kwani huingiwa na hofu. 

Lakini pia  Jamii zinazoishi wilaya ya Mkoani wanaishi kijamii kwa maana wengi ni ndugu tofauti na Wilaya ya Chake yenye wahamiaji wengi". 

ni  maneno ya  Wakili wa Serikali  kutoka ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka  Pemba Ali Amour Makame  

Jeshi la Polisi  linadai  kutokana na changamoto hiyo hulazimika kutumia  askari wakaguzi  ambao wamekuwa mbadala wa kuimarisha ulinzi na usalama  katika shehia ambazo zipo mbali na kituo hicho cha Polisi. 


" Tunao maafisa wakaguzi ambao tumewaweka maalum katika  kila  shehia kuona kwamba wanaimarisha  na kutoa mashirikiano   juu ya kutatua changamoto mbali mbali katika kuimarisha ulinzi" 

" Changamoto iliyopo kwa sasa  bado tuna uhaba wa askari hao na tunashughulikia  kuona kwamba wanatosheleza   bado askari mmoja hulazimika kusimamia shehia zaidi ya tatu".

" Kuhusu Suala la vituo ni jambo la Jamii husika watakapoona kuna ulazima wa kuwepo Jeshi halitosita kupeleka askari vituoni humo. 

Hivyo ni jambo la kukaa na kujadilina uongozi wa wilaya kuona namna gani wanafanikisha hilo sababu  jukumu letu ni kuimarisha ulinzi na usalama na askari wetu wapo tayari". 

Maneno kutoka kwa  Kamishna Wa Polisi Zanzibar Hamad Khamis Hamad. 

UNGOZI WA WILAYA UNASEMAJE

Masheha waliowengi  mara kwa mara katika vikao vyetu wamekuwa wakiligusia suala hili  na sisi uongozi tayari tumeanza kulijadili   katika vikao vya mkoa  kuona   vipi tutalipatia ufumbuzi suala hili. 

 kutokana na ukuaji wa miji, na ongezeko la idadi ya watu  kwa wilaya yetu ya chake chake sasa ivi bado tuna kituo kimoja tu cha polisi

"Miji yetu inakuwa zaidi, watu wanaongezeka, harakati za kiuchumi za kijamii pia zinakua, ni kiri kuwa kituo hichi hakitoshelezi hivyo  ni wazi kuwa ipo haja ya kuongeza vituo  hivyo ili kudhibiti  zaidi usalama  zaidi. 

 "Bado uongozi wa wilaya mpaka sasa haujafanikisha suala hilo  la ujenzi  wa vituo vyengine vya polisi katika maeneo mbali mbali ya mji wa Chake Chake. 

 Tumebahatika kupata barabara kubwa hii ya ole kengeja ambayo imekuwa na tija kubwa  na wananchi wameanza kuvutika kuanza kuishi katika ukanda wa barabara. 

Lakini bado utakuta ole mpka kufika kengeja bado hakuna  kituo cha Polisi ni maeneo muhimu ambayo pia yana umuhimu na ulazima wa kuwepo na  kituo". 

"Serikali ya wilaya tayari imetenga maeneo maalum ambayo itakuwa tayari kuyatumia kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya Polisi katika wilaya hiyo endapo serikali kuu itaridhia   na  wadau watajitokeza kujenga vituo hivyo katika wilaya ya chake chake. 

 Aidha amesema  uongozi wa Wilaya  unaendelea  kuzungumza na wadau na wazalendo wa nchi ili kupata msaada wa kujengewa  vituo vya polisi katika badhi ya maeneo muhumu na yenye ulazima wa kuwepo  vituo vya polisi   katika wilaya hiyo. 

" Chake  ina zaidi ya bandari zisizo rasmi 88  ambazo wahalifu huzitumia   jeshi la Polisi linaendelea kudhibiti na kukamata   wanaotumia  maeneo hayo  lakini  shida ni kukosekana  kituo maeneo yakaribu na bandari hizo. "

"Wezetu wilaya ya Mkoani wana vituo  vingi  hata kasi yao ya kudhibiti vitendo vya kihalifu inaongezeka  maeneo yao ya bandari kuna kituo, Kengeja, Mtambile  na mote humo ukaguzi unakuwa unafanyika. 

na kunazuilika uhalifu  unapotokezea kwa upande wa mashariki kituo kipo karibu  magharibi lakini pia center ya mji kipo kituo karibu,kadhalika wete na micheweni Alisema". 

" Kituo kipo Mjini  lakini kuna maeneo ambayo ufikiaji wake ni mgumu kwa mfano  Mgelema,  kilindi Ndagoni ni mbali na yote ni maeneo ambayo  kuna bahari, kote huko kwa umuhimu wake kunastahiki kabisa kuwa na vituo vya polisi. 

 Abdalla Rashid aliwataka wananchi kutosita kuisadia Serikali na jeshi la Polisi kudhibiti vitendo vya kihalifu endapo watabaini kuwepo kwa vitendo viovu katika jamii zao kwa kutoa taarifa. 

" Tuko Tayari kutoa mashirikiano  kwa yeyote atakaekuwa tayari kusaidia suala hili la ujenzi wa vituo vya polisi katika wilaya yangu. 

Wadau wa kupinga udhalilishaji, kulinda haki za binaadamu watu binafsi kikundi cha watu  taasisi za fedha   na wasamaria wema  wajitokeze kufanikisha  kupunguza changamoto hii lengo ni kuona tunaendeleza mapambano ya kudhibiti uhalifu wa aina mbali mbali. "

Wilaya ya Chake Chake ina shehi 32 Ambazo ni  Shehia ya  Wara, Kichungwani, Chanjaani, Matale,  Kilindi, Kibokoni, Uwandani, Ng'ambwa, Wawi, Mchanga Mrima, Ndagoni, Wesha, Birikau, Madungu, Shungi, Msingini, Chachani, Mgelema,  Tibirinzi, Kwale, Michungwani, Gombani, Vitongoji, Mfikiwa, Mgogoni, Ole, Mjini ole, Mbuzini, Mvumoni, Pujini, Chonga Pamoja na Chanjamjawiri

Shehia zote hizo zimekuwa zikiendelea kuishi kwa wasi wasi endapo vitajitokeza vitendo vya kihalifu nyakati za usiku ambapo  Wananchi  wengi wanaoishi   katika baadhi y vijiji vilivyomo ndani  shehia   hizo hushindwa kuripoti matukio ya kiuhalifu huku wengine kuripoti matukio mara moja  bila kuyafuatilia sababu ikiwa  ni umbali wa vituo vya Polisi. 

 Suala hili hupelekea kukosa haki zao muhimu huku watoto  vijana na wanawake  wakiendelea kukosa haki zao muhimu kutikana na kufanyiwa  vitendo vya kikatili ikiwemo udhalilishaji jambo ambalo hupelekea kuvunjwa  sheria mbali mbali ya usalama wao Huku shehia moja ya Madungu  ikibakia kuwa Salama   Juu ya mapamabo dhidi ya uhalifu. 

Waswahili wanasema "Usipoziba Ufa Utajenga Ukuta  " Wakiwa na maana ya  tahadahari  ya mapema  juu ya kudhibiti Tatizo dogo kuwa kubwa  hivyo natamani kabla hakujatokea  maafa  kutokqna na upungufu huu  Ufa huu uonekane katika kuendeleza mapambano ya kutunza na kulinda haki za binaadamu.

 Huku wengine wakisema kuwa " Kinga ni bora kuliko tiba"  na  kumalizia kwa kusema usipoziba ufa utajenga ukuta.  yote haya huenda yakaja kuleta madhara  endapo suala hili halitochukuliwa hatua. 

Mwisho. 

Comments

Post a Comment

Popular posts from this blog

BARABARA 19 KUJENGWA KWA KIWANGO CHA LAMI PEMBA KUKAMILIKA DISEMBA 2024.

WAZAZI ZIDISHENI KUFUATILIA NYENENDO ZA WATOTO HUSUSAN NI VIJANA .

UONGOZI WA WILAYA CHAKE CHAKE KFHI WAPONGEZA JUHUDI