WANANCHI KISIWA CHA KOJANI WALILIA KUKOSA MADAKTARI KITUO CHAO CHA AFYA
Na - AMINA AHMED, PEMBA.
Wametoa ombi hilo walipokuwa wakizungumza mbele ya kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa huo uliofika kisiwani humo kusikiliza changamoto zinazowakabili wananchi ndani ya kisiwa hicho mapema leo.
Wamesema kituo cha afya ndani ya kisiwa hicho kina daktari mmoja ambae wakati mwengine kushindwa kutoa huduma kwa baadhi ya kesi za matibabu zinazofika kituoni humo huku akilazimika kutoa huduma kwa wagonjwa zaidi ya 80 kwa siku .
Aidha wameomba kupatiwa ufumbuzi wa changamoto ya kukosa maji safi katika baadhi ya maeneo iliyokosekana kutokana na kuharibika kwa muda mrefu tangi lilikokuwa likisambazia maji katika maeneo mbali mbali ya vijiji hivyo .
Katika hatua nyengine wananchi hao wameiomba serikali ya mkoa kuwasaidia kudhibiti mmonyoko wa maadili kwa kuridhia sheria zitakazowekwa na kamati ya maadili kisiwani humo .
Kwa upande wake mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama mkoa wa Kaskazini Pemba ambae pia ni mkuu wa mkoa huo Salama Mbarouk Khatib amesema kuwa ataendelea kulifanyia kazi suala hilo kwa kulifikisha kwa uongozi wa wizara ya afya ili kuona linapatiwa ufumbuzi wa haraka na uongozi wa wizara ya afya kwa maslahi ya wananchi.
Aidha amewataka akina mama wa kisiwa hicho kujifungulia hospitali sambamba na kuhudhuria kliniki wakati wa ujauzito ili kuepusha athari zinazoweza kujitokeza endapo watajifungulia majumbani mwao.
Akijibu kuhusu changamoto ya upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama mkuu huyo aliwahakikishia wananchi hao kuwa suala hilo litapatiwa ufumbuzi siku ya jumamosi ni baada ya kuzungumza hadharani kwa njia ya simu uongozi wa mamlaka ya maji Zanzibar zawa na kutoa ahadi hiyo.
Aidha akizungumzia suala la maadili mwenyekiti huyo amewataka wazazi kusimamia na kufuatilia mienendo ya vijana na watoto ili kuwaepusha kujiingiza katika vitendo viouvu.
Katika hatua nyengine Rc Salama ameagiza kukatwa nywele kwa vijana wakiume wanaofuga na kusokota rasta, kuvaa nguo za kubana na kuzishusha suruali zao sambamba na kuwataka kuacha mara moja tabia hizo ambapo amesema pia uongozi wa mkoa utawashughulikia ipasavyo
ili kurudisha nidhamu ya maadili.