WANANCHI CHAKE CHAKE WAASWA MASHIRIKIANO KUGUNDUA WAGONJWA WAPYA WA KIFUA KIKUU.
AMINA AHMED MOH'D.
WANANCHI wa wilaya ya Chake Chake wametakiwa kutoa mashirikiano kwa kwa wataalamu wa afya ambao wataendeleza zoezi la kuwafuatilia wagonjwa wapya wa kifua kikuu (TB) ili lengo la kuinusuru jamii juu ya ugonjwa huo liweze kufikiwa .
Kauli hiyo ya mkuu wa wilaya wa Chake Chake Abdalla Rashid Ali imetolewa kwa niaba yake na Mkuu wa wilaya ya Mkoani Khatib Juma Mjaja alipokuwa akizungumza nao katika mkutano wa ufunguzi wa mradi wa miezi 15 wa kuimarisha ufuatiliaji wa wagonjwa wapya kifua kikuu ( TB ) katika jamii (TBCI ) unaotekelezwa na jumuia ya wauguzi "Zanzibar Nurses" Association ( ZANA ) huko katika ukumbi wa maabara ya afya ya jamii ( PHL ) Wawi mapema leo.
Amesema lengo la serikali kuruhusu jumuia binafsi kutekeleza shughuli za kitaaluma ni kuweza kusaidia kuona changamoto katika masuala tofauti ikiwemo masuala ya afya na kuweza kusaidiana nao katika kuleta mageuzi katika jamii hivyo mashirikiano hayo yatasaidia kuweza kuwagundua wagonjwa wapya na kupata matibabu kwa urahisi .
" Ugonjwa wa TB bado ni changamoto hususan ni kwa vijana hivyo ni waase wananchi Chake chake na kusini yote kutoa mashirikiano katika kuona ugonjwa huu unadhibitiwa kwa kupatiwa tiba.
Aidha mkuu huyo ameipongeza jumuia ya wauguzi zana kwa mradi huo ambao unalengo la kuisaidia serikali katika kuimarisha afya za wanachi wake .
"Serikali kuu haiwezi kutekeleza kila kitu ZANA wameona changamoto hii ya ugonjwa wa kifua kikuu TB ambayo haipo wilaya ya Chake chake tu takriban dunia nzima inaugonjwa huu tunashukuru kwa kuasisi mradi huu ambao unakwenda kuwagusa wananchi moja kwa moja huku ikigusa dhamira njema ya Rais wa Zanzibar Dk Hussein Ali Mwinyi katika kuimarisha huduma za matibabu nchini.
Hata hivyo ametaka wanajumuia hiyo kuzidisha kutoa elimu juu ya ugonjwa huo wa ( TB ) kwa wanajamii ili waweze kuzijua dalili zake na namna ya kijikinga.
Akizungumza kuhusu utekelezaji wa mradi huo Msaidizi mratibu wa mradi huo wa kuwagundua wagonjwa wapya katika jamii Mwajuma Ali Shehe amesema utekelezaji wa mradi huo uliofadhiliwa na ( J S I ) unatarajiwa kuibua wagonjwa 2720 katika wilaya hiyo ambao wanatarjiwa kufanyiwa uchunguzi kupitia familia na jamaa wagonjwa wa TB maeneo mbali mbali ya wilaya hiyo ili kupatiwa tiba.
Awali akizungumza katibu wa Jumuia ya ZANA Pemba Othman Bakari Mohamed amesema jumuia hiyo imekuwa msatari wa mbele katika kutekeleza miradi mbali mbali ya kijamii ambayo inalengo la kuleta mabadiliko ya kiafya katika jamii .
Shehia 10 ndani ya wilaya ya Chake chake ambazo zinatarajiwa kunufaika na mradi huo wa kuwagundua wagonjwa wapya wa Kifua kikuu katika jamii kwa awamu ya kwanza ambapo Utekelezaji wa mradi huo unatafanyika katika mikoa miwili ya Zanzibar ikiwemo mkoa wa mjini maghrib pamoja na mkoa wa Kusini Pemba huku Shehia nyengine kumi kwa upande wa wilaya ya Mkoani zikitarajiwa kunufaika na mradi huo .
Aidha mada juu ya kifua kikuu pamoja na kifua kikuu sugu ni miongoni mwa mada zilizofundishwa kwa wadau hao wakiwemo viongozi wa shehia ,viongozi wa dini,wauguzi,wasimamizi wa vituo vya afya vya serikali na binafsi watu wenye ulemavu ndani ya wilaya hiyo wameshiriki katika mkutano huo huku mkutano kama huo kwa wadau kutoka wilaya ya Mkoani ukitarajiwa kufanyika kesho.
Mwisho
Comments
Post a Comment