PEMBA PRESS CLUB YAADHIMISHA SIKU YA UHURU WA VYOMBO VYA HABARI MATTAR AWATOA HOFU AAHIDI MASHIRIKIANO ZAIDI KWA WAANDISHI.
NA , AMINA AHMED MOH'D- PEMBA.

UONGOZI wa Mkoa Kusini Pemba umesema utaendelea kutoa mashirikiano kwa waandishi wa habari kisiwani humo ili kuweza kurahisisha utendaji wa kazi zao za kila siku na kuleta mabadiliko katika jamii juu ya mambo mbali mbali.
Kauli hiyo imetolewa na mkuu wa mkoa huo Mattar Zahor Massoud alipokuwa akifungua mkutano maalum wa maadhimisho ya siku ya uhuru wa vyombo vya habari uliandaliwa na Club ya waandishi wa Habari Pemba ( PPC ) uliofanyika katika ukumbi wa Samail Gombani Chake Chake mapema leo .
Amesema maelezo na ufafanuzi juu ya mambo mbali mbali yanayohusu maendeleo ya wananchi yanaweza kufikiwa iwapo waandishi wenyewe kisiwani humo watakuwa tayari kuitumia fursa hiyo ya mashirikiano katika kutafuta taarifa kutoka kwa vyanzo sahihi .
Aidha mkuu huyo akaitumia nafasi hiyo kuwataka waandishi wa habari kuandika habari zitakazoelimisha jamii juu ya kuhifadhi mazingira kwa nadharia ya kutunza urithi wa kijani sambamba na habari zitakazobadilisha jamii juu ya suala hilo katika hatua za awali.
Mattar akatumia fursa hiyo pia kuwaasa waandishi wa habari kisiwani humo kujiendeleza zaidi kielimu ili kujiongezea fursa na maarifa katika kutenda kazi ya habari kwa ufanisi na uweledi.
Amesema iwapo waandishi wataendelea kuongeza ujuzi katika taaluma hiyo kutasaidia jamii kuweza kuwatofautisha waandishi wenye uweledi na makanjanja wanaovamia tasnia hiyo na kuwaharibia sifa zao kwa kukiuka maadili ya habari.
Kwa upande wake Afisa mdhamini wa wizara ya habari Pemba Mfamau Lali Mfamau amewataka waandishi wa habari hao ambao ni wanachama wa Pemba Press Club kuendelea kusimamia nidhamu na kutojihusisha kuwa sehemu ya kuvunja nidhamu zilizowekwa na taasisi zinazosimamia tasnia hiyo.
Akizungumza Katika Mkutano wa maadhimisho hayo yaliobeba ujumbe wa Uandishi wa habari kwa Mabadiliko ya Tabia ya nchi Mwenyekiti wa Pemba Press Club PPC Bakar Mussa Juma amesema wanachama wa club hiyo wataendelea kushirikiana na taasisi yeyote katika kuleta maendeleo kwa wananchi juu ya mambo mbali mbali.
Tamati ya maadhimisho hayo mwaka huu wanachama wa club hiyo wanatarajiwa kupanda miti katika eneo la Kambini kichokochwe ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono utunzaji wa mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya Tabia ya nchi.
Mwisho.
Comments
Post a Comment