KUPASUKA BARABARA KUFANYIWA UTAFITI PEMBA
NA AMINA AHMED MOH’D, PEMBA.
WIZARA ya Ujenzi Mawasiliano na Uchukuzi Zanzibar imesema itaendelea kuchukua hatua za dharura kuzifanyia marekebisho ya haraka barabara zote za kisiwani Pemba zilizoharibika kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha ili kuwaondoshea Usumbufu wananchi wake.
Waziri wa wizara hiyo Khalid Salum Mohamed ameyasema hayo huko Makombeni Darajani wilaya ya Mkoani alipokuwa akizungumza na kutoa ufafanuzi kwa kamati ya Mawasiliano Ardhi na nishati iliofika na kutembelea ujenzi wa barabara mbali mbali na kujionea mtengenezo kwa baadhi ya barabara zilizokatika kutokana na mvua ikiwemo barabara hiyo.
Amesema kupasuka na kukatika kwa barabara nyingi kisiwani Pemba mara zinapopata mvua ni kutokana na aina ya udongo uliopo katika ardhi nyingi kisiwani humo jambo ambalo wizara linaendelea kuzifanya utafiti wa kitaalamu kujua chanzo hasa kinachopelekea kupasuka kwa barabara mbali mbali, huku matengenezo ya dharura yakiendelea kuchukuliwa kuzitengeneza .
Aidha amesema licha ya kukamilika kwa hatua ya kwanza ujenzi wa barabara ya Kipapo Mgelema wambaa, na kushindwa kukamilika moja kwa moja barabara hiyo kwa wizara inaendelea na ujenzi ili kukamilika kwa hatua zilizobakia ndani ya bara bara hiyo.
"Wizara inaendelea na hatua mbali mbali za ujenzi wa barabara hii tumeshakamilisha kwa asilimia 90 baadhi ya maeneo na mengine yaliobaki ni hatua za mwisho kwajili ya kuweka lami ili kukamilika, Changamoto mbali mbali zilijitokeza lakini wizara zimesimamia kuzipatia ufumbuzi na wananchi hivi karibuni watazidi kuitumia barabara hii ikiwa imeshakamilika".
Amesema kuchelewa kukamilika kwa ujenzi wa barabara mbali unguja na Pemba kumetokana na changamoto mbali mbali ambazo wizara imeshazichukulia hatua ili kuzikamlisha kwa wakati na wananchi kuweza kuzitumia kwa shughuli mbali mbali.
Alisema kwa upande wa ujenzi wa barabara za vijijini kisiwani humo wizara inaendelea na ujenzi katika maeneo mbali ili kuendelea kufikisha huduma za usafiri katika vijiji na kurahisisha upatikanaji wa maendeleo ambapo asilimi 98 ya barabara hizo upande wa kusini zimeshafanyiwa usafi kwajili ya matengezo .
Hata hivyo Dk Khalid amesema kuwa wizara imetoa zaidi kipaumbele kwa barabara 3 kisiwani humo katika kuhakikisha zinajengwa na kukamilika kwa wakati.
Hata hivyo alisema kuwa Matengenezo ya barabara hizo ni pamoja na uwekaji wa mitaro, pamoja na alama za barabarani katika kuhakikisha haziathiriki na kuharibiwa na mvua.
Akizungumza makamo mwenyekiti wa kamati ya Mawasiliano Ardhi na nishati ya baraza la wawakilishi Aza Januar Joseph ameipongeza wizara hiyo kwa kuendelea na ujenzi wa barabara mbali mbali na nyengine kukamilika licha ya kukabiliwa na changamoto za fedha pamoja na baadhi ya vifaa vya kutendea kazi.
Aidha Aza Amesema kamati hiyo imeridhishwa na majibu sambamba na kujionea maendeleo yaliofikiwa na wizara hiyo katika ujenzi wa barabara mbali mbali kisiwani Pemba .
Tumeona mambo mbali mbali tumeona shughuli zinavyokwenda za ujenzi wa matengenzo ya barabara tunaipongeza sana wizara kwa kazi wanazofanya, Tumeona kwamba hatua za dharura zinachukuliwa za kudhidbiti tatizo ambalo limeonekana limaweza likaleta athari ambazo zinaweza kuzuia njia zisiweze kupitika.
Kwa Upande wake Afisa mdhamini wizara ya Mawasiliano Ujenzi na uchukuzi Pemba Ibrahim Saleh Juma Amesema kuwa ucheweshwaji wa ujenzi wa barabara mbali mbali kisiwani Pemba kunatokana na uhaba wa vifaa pamoja na rasilimali fedha ambapo hatua za kulipatia ufumbuzi suala hilo zimeshachukuliwa kiwemo kuwasilisha mpango kazi wizara ya fedha na mipango kwajili ya upatikanaji wa fedha na mara zitakapokamilika suala hilo litapatiwa ufumbuzi kwa muda mfupi.
Kamati hiyo imetembelea barabara mbali mbali kusini Pemba ikiwemo Ukutini Mtangani, Ole Kengeja, Makombeni Mkoani, Chanjaani Puniji.
Comments
Post a Comment