MIKAKATI YA KUDHIBITI UTORO YAZAA MATUNDA.

HII HAPA MIKAKATI YA UFAULU NA KUDHIBITI UTORO SKULI ZA MSINGI MICHEWENI

Na Amina Ahmed Mohamed

MIKAKATI iliyobuniwa na uongozi wa wilaya ya Micheweni kudhibiti utoro skuli za msingi wilaya ya Micheweni imewezesha wilaya hiyo kuongoza kitaifa kwa ufaulu kwa miaka minne mfululizo.


Mkuu wa wilaya ya Michewemi Mgeni Khatib Yahya amesema mikakati hiyo ni pamoja na   kupiga marufuku ajira za watoto maeneo yote na wananchi katika shehiza zote kwenye wilaya hiyo wameelimishwa kuzingatia umuhimu wa elimu na malezi bora,

Kadhalika wilaya ya Micheweni imeunda kamati maalum katika kila shehia kufuatilia suala la suala la utoro skuli na imepepiga marufuku watoto wa skuli kushiriki dufu la usiku na kuzunguka hovyo usiku kuangalia televisheni.

Tatizo la dufu linathibitishwa na mkazi wa shehia ya Majenzi Hassan Omar ambaye anasema "zamani watoto walikuwa wanachelewa kulala wanazifuata ngoma popote zinapopigwa hawakataziki lakini aliekuwa mkuu wa wilaya alipotoa marufuku waliogopa wakaanza kutulia majumbani kusoma”.

Kwa mujibu wa   mkuu wa wilaya ya Micheweni  alipoanza kazi katika  wilaya hii mwaka 2020 kulikuwa na jumla ya wanafunzi watoro 7,609  ambao walikuwa nje ya skuli ambapo 3,000 kati yao ni wanafunzi wa skuli za msingi . 

Amesema hata hivyo wanafunzi 1,240 wakiwepo wanawake 892 na wanaume 348 wamesharudishwa skuli rasmi na wanaendelea vema na masomo.

Afisa Elimu msingi wilaya ya Micheweni Asya Msellem Hassan amesema   utoro uliobaki wilaya ya Micheweni kwa sasa sio ule wa moja kwa moja unatofautiana na ule wa miaka iliyopita   huku zaidi ukibaki katika maeneo ya ukanda wa pwani. 

 "Upo ule utoro wa siku mbili siku moja bhasi na zaidi ni skuli ambazo zipo maeneo ya bahari Makangale, Tumbe, Shumba Maziwa ng'ombe na hivyo sio ule wa mtoto kukatisha moja kwa moja  mkuu wa wilaya anatusaidia  kazi hii ya kumaliza utoro Micheweni".

SHEHA WAFUNGUKA

Ili kupata kufahamu kinachoendelea kwenye shehia kuhusu mikakati ya kudhibiti utoro skuli mwandishi alifunga safari hadi Sheha wa Makangale na kuzungumza ana kwa ana na sheha wa shehiya hiyo Said Kombo Said ambaye amesema; 

"Utoro ulikuwepo kutokana na suala la maji wanafunzi walikuwa wanatumia kisingizio cha  kufuata maji ya bomba  na kutoroka skuli na  kushuka baharini  kwenda kufanya kazi za kupara samaki,  kuokota Mwani na au kwenda ucheza badala ya kwenda skuli.

Sheha huyo amesema kwa sasa ‘’mashirikiano ya kamati iliyoundwa shehiani petu na wanakijiji hasubutu mwanafunzi kutoroka wanagopa wakionekana watachukuliwa hatua’’. 

Amema tatizo limepungua sana  na kwamba mkuu wa wilaya anapita pita na anatoa maelekezo  wanashirikiana bega kwa bega kutekeleza maelekezo hayo.   .

Sheha huyo wa shehia ya Makangale amesema katika shehia hiyo imeweka sheria ambapo mzazi atakaeonekana anamtumikisha mtoto atachukuliwa hatua.

Kwa upande wake, Rahila Ramadhan Juma Sheha wa shehia ya Shumba Mjini ameeleza hali ilivyokuwa awali kuhusu utoro skuli na mikakati ya kudhibiti tatizo hilo ilivyofanikiwa. 

 ”Suala la utoro ilikuwa ni uelewa mdogo wazazi juu ya umuhimu wa elimu ndio husababisha wanafunzi washindwe kudhibitiwa wanakuwa wapo majumbani mwao”, anaeleza sheha Rahila. 

Amesema kwa mfano awali wazazi walikuwa hawako tayari kutoa mashirikiano kumaliza tatizo la utoro wala kusimamia wanafunzi wasome.

Hata hivyo amesema utoro pia ulikuwa unachangiwa na tatizo la uchache wa waalimu walimu mashuleni. “Utakuta mwalimu mmoja anashghulikia darasa moja lenye wanafunzi pengine 70 wale atawadhibiti lakini madarasa mengine huku hayana mwalimu hayasimamiwi wanatoroka kwa vile vipindi zaidi ya vitatu darasa halijaingia mwalimu", amesema

 "Hali ya ufaulu mfano awali skuli yaa msingi iliyopo Shehiani mwangu Skuli ya Karume ilikuwa haitoi wanafunzi waliofaulu michipuo lakini mwaka jana 2021 ilitoa ni jambo la faraja".

Kwa upande wake Sheha wa shehia ya Micheweni Khadija Abdi Haji  Kuhusi  alipofikiwa  na kuhojiwa alisema  "nikiri utoro kwa wanafunzi wa skuli za msingi limefanikiwa kudhibitiwa na ni  kutokana na kamati maalum ya kusimamia utoro wa wanafunzi   na tumefanikiwa juu ya hilo na leo hii limepungua kabisa".

WANAFUNZI WATORO WALIORUDISHWA SKULI

 Baadhi ya wanafunzi ambao  uongozi wa wilaya  walifanikiwa kuwarudisha skuli wametoa duku duku lao  walipokuwa nje ya  skuli  ambapo wamedai  sababu ya kutoroka skuli ni kutokana na kukosa  sare, kuumwa pamoja na kukosa ufahamu katika masomo yao.

Heri Omar amesema "nilijiona sifahamu masomo ya skuli nikawa nje ya skuli lakini kwa sasa nimesharudi nawaambia wanafunzi wengine ambao wametoroka warudi skuli tuje tusome’’.

Mwanafunzi mwingine Time Makame amesema “nilikuwa sina sare kwa sasa nishapata naawambia wanafunzi wenzangu warudi skuli waje tuje tusome elimu ni ufunguo wa maisha’’.  

Kwa upande wake mwanafunzi Fatma Juma Ali anasema alikuwa anaumwa na kifua   kwa sababu alikuwa anabanja mawe  ya kokoto na  ndiyo sababu  akawa haende skuli  lakini kwa sasa ‘’nisharudi nawaambia wanafunzi wenzangu wasikae utoro waje skuli tusome tupate  kufanikiwa" . 

WALIMU WAELEZA MIKAKATI YAO

Walimu  kwa upande wao WAELEZA kuwa  kufanikiwa kwa jitihada za kudhibiti utoro kwa wanafunzi  kumetokana na vikao vya walimu wakuu  wa skuli zilizomo ndani ya wilaya kupanga mikakati ya pamoja  ili kuona tuna ufaulu haushuki. 

"Mikakati ikiwemo ya walimu wakuu kuanzisha kambi za kusoma muda wa ziada, kamati maalum za skuli kufuatilia watoro jambo ambalo tumefanikiwa kupunguza taatizo la utoro lakini kuongeza ufaulu", amedokeza Salum Mkadam Hamad mwalimu mkuu Skuli ya Mkanagale Msingi. 

 Kai Omar Haji kutoka skuli ya Micheweni B msingi amesema kambi za kimasomo zina mchango mkubwa na kuwa chachu ya maendeleo ya elimu na silaha ya kudhibiti utoro. Amesisitiza kuwa   ‘’lazima walimu tujue mwenendo wa mwanafunzi   tunakuwa nao muda wote hilo linasababisha utoro usijitokeze kwa sana"


ONGEZEKO LA UFAULU

‘’Kuna msemo usemao penye nia pana njia’’ Msemo huu umethibitika katika Wilaya ya Micheweni kufuatia takwimu zilizotolewa na Afisa Elimu msingi wilaya ya Micheweni Asya Msellem Hassan zinazoonyesha kwamba mwaka 2019 jumla  ya wanafunzi 107 walifaulu  kati ya wanafunzi 1632 ambao walifanya mitihani ya darasa la sita wilayani humo. 

Amesema ufaulu uliongezeka zaidi mwaka 2020 ambapo   jumla ya wanafunzi 1919 waliofanya mitihani 167 kati yao walifaulu   jambo ambalo  kabla halijawahi kutokea.  

Ameongeza Mwaka  2021  wanafunzi 257 walifaulu kati ya wanafunzi  3255 waliofanya mitihani skuli  za msingi wilaya hiyo.

Wilaya ya Micheweni  iliyoko  katika Mkoa wa kaskazini ndani ya kisiwa cha  Pemba ambayo ni moja ya wilaya kumi zilizoko  Zanzibar inaongoza kwa matokeo  ya darasa la nne sambamba na kuvuuka lengo  liliowekwa na wizara ya Elimu  juu ya kudhibiti tatizo la  utoro na kuwarejesha skuli wanafunzi wa skuli za msingi waliotoroka kwa sababu mbali mbali.

 mwisho

 

Comments

Popular posts from this blog

BARABARA 19 KUJENGWA KWA KIWANGO CHA LAMI PEMBA KUKAMILIKA DISEMBA 2024.

ZSTC YAWAONYA WAUZAJI NA WANUNUAJI KARAFUU KINYUME NA UTARATIBU ULIOWEKWA .

WIZARA YA AFYA YAWAPA UJUMBE HUU VIONGOZI WA DINI KUUFIKISHA KATIKA JAMII