MABADILIKO WATENDAJI ZRA PEMBA WALETA MATUMAINI KWA WAFANYA BIASHARA

NA, AMINA AHMED MOH’D - PEMBA. 
BAADHI ya Wafanya Biashara  wilaya ya  Mkoani  mkoa wa Kusini Pemba wamepongeza juhudi zinazoendelea kuchukuliwa na mamlaka ya mapato Zanzibar ZRA  juu ya maswala ya utolewaji wa  elimuya kodi  na hatua za ukusanyaji wa mapato   ukilinganisha  miaka iliyopita. 

  Kauli  hizo zimetolewa na wafanya biashara  kutoka mitaa na maeneo mbali mbali ya wilaya hiyo   walipokuwa wakizungumza  mbele ya Mkurugenzi wa Mamlaka ya Mapato Zanzibar ZRA Pemba Jamal Hassan Jamal aliefika  ndani ya wilaya hiyo   kuzungumza na kusikiliza changamoto za wafanyabiashara maeneo tofauti ikiwa ni mwezi maalum wa kurejesha shukurani kwa walipa kodi ulioandaliwa na  mamlaka hiyo.

 Wamesema suala la utolewaji wa taaluma juu ya njia  sahihi za ulipaji kodi zimeimarika na jambo ambalo awali lilikuwa  ni changamoto kubwa  kwa wafanya biashara na watendaji wa mamlaka hiyo katika kukusanya mapato.

 Tunashukuru ZRA  Pemba  watendaji wamebadilika  tofauti na awali uelewa na taaluma wanazidi kutupatia kila tunapohitaji,wamekuwa  karibu sana na sisi    wamekuwa marafiki ambao wanatuhamasisha kuwa walipaji kodi kwa hiari zile vuta ni kuvute zimepungua". Alisema  Yussuf Mussa Makame Mfanya biashara wa saruji, pamoja na mbao   Mkoani . 

Aidha  Wafanya biashara hao wameiomba mamlaka hiyo  kuwashirikisha  kunapotokea mabadiliko  katika taratibu mbali mbali za ulipaji a kodi. 

 " Tumezipokea shukurani  zenu hizi kwa mikono miwili  na sisi tunaahidi tutaendelea kuiunga mkono serikali kwa kuwa  walipa kodi  wazuri,  kodi ambazo zinarudi kwetu kufanya maendeleo mbali mbali".

"Kunapotokea mabadiliko yeyote mtushirikishe sisi wafanya biashara kwa sababu hatuna lengo la kukwepa kulipa kodi  sote tunajenga nyumba moja  hivyo mabadiliko yanayotuhusu walipa kodi msiyakalie kimya   yakitokea mtuambie ili mnapofanya mabadiliko  tusiwe tunalalamika".alisema mfanya biashara Said  Hemed 

 Katika Hatua nyengine  wafanya biashara hao wameishukuru Serikali ya awamu ya 8   kwa kuendelea  kuleta maendeleo  katika wilaya hiyo ikiwemo ujenzi wa masoko, uimarishwaji wa  bandari kutoa fursa kwa  wafanya biashara, na kuwakubalia maombi yao katika kuwekeza na kujenga vyanzo vipya vya  kufanyia biashara.

"Maendeleo ya wazi wazi tunayaona sisi kama wafanya biashara kwetu hili ni jambo la faraja  tunapata moyo zaidi katika kulipa kodi, tunaona barabara zinajengwa, mahospitali na vifaa, bandari masoko vyote hivyo ni kwa muda mchache wa awamu hii ya nane tunatamani rais wetu akae  siku zote  asiondoke tena kwa sababu kile kilio tulichokuwa tunalia zamani kimeondoka tulikuwa tunalilia maendeleo na yamekuja kwa kasi na yanaendelea"alisema Hemed Muhammed mfanya biashara wa Vifaa vya ujenzi na vyombo vya moto.

Mkurugenzi wa ZRA Pemba Jamal Hassan Jamal Amesema lengo la  kutembelea walipa kodi wa hiari waliofanya vizuri katika wilaya hiyo kwa mwaka 2023 ni kurejesha shukurani kusikiliza changamoto sambamba na kupokea maoni  katika kuimarisha zaidi utendaji kazi wa mamlaka hiyo.

Aidha  Jamal amesema mamlaka hiyo itaendelea kushirikiana vyema na walipa kodi katika kuona malengo yaliowekwa na serikali juu ya kuboresha maendeleo katika  nyanja mbali mbali  yanafikiwa.

  Hata hivyo amewataka wafanya biashara kuendelea kutoa mashirikiano na mamlaka hiyo   ikiwa ni pamoja na kutoa taarifa wanapokabikiwa na changamoto mbali mbali  juu ya mifumo ya ulipaji kodi.

  Miongoni mwa maduka hayo yaliotembelewa ni Pamoja na Maduka ya biashara za vyakula, vipodozi, mbao, Saruji, Nguo na  mengineyo kutoka maeneo mbali mbali ndani ya wilaya hiyo.

 Mwisho

Comments

Popular posts from this blog

BARABARA 19 KUJENGWA KWA KIWANGO CHA LAMI PEMBA KUKAMILIKA DISEMBA 2024.

WAZAZI ZIDISHENI KUFUATILIA NYENENDO ZA WATOTO HUSUSAN NI VIJANA .

UONGOZI WA WILAYA CHAKE CHAKE KFHI WAPONGEZA JUHUDI