WIZARA YA AFYA PEMBA YATOA NENO KWA WANAOSAMBAZA UVUMI KUHUSU MAGONJWA YA MIRIPUKO.

NA AMINA AHMED MOH'D, PEMBA. 

WIZARA ya Afya Zanzibar imewataka  waandishi wa habari pamoja na wahudumu wa Afya ya jamii CHV kungana  pamoja  katika kuiweka salama jamii  juu ya majanga ya miripuko  mbali mbali  kwa kuelimisha na kutoa taarifa  kutoka kwa  vyanzo vyenye usahihi  ili kuepusha mitafaruku inayowapata wananchi kutokana na uvumi hususan katika msimu wa mvua zinazoendelea  kunyesha. 

 Kauli hiyo imetolewa na  Afisa Mdhamini Wizara ya Afya Pemba Khamis Bilali Ali alipokuwa  akizungumza na baadhi ya wanahabari   wa vyombo mbali mbali pamoja na wahudumu wa Afya jamii CHV kiswani Pemba  katika mafunzo maalumu juu ya kudhibiti kusambaa kwa uvumi na maneno mbali mbali katika vipindi vya majanga  huko Samail Gombani Chake. 

Amesema  makundi hayo yanayonafasi kubwa katika kusaidia jamii kuwa na uwelewa wa kutofautisha uvumi   na taarifa potofu kwa kuweka usahihi kwa jamii  na kuwaepushia hofu ambayo hupelekea  taharuki kwa wananchi. 

"Mtaani humo kunatolewa taarifa tofauti, watu wanatunga tu mambo mara mvua zimeanza  wagonjwa wakipindupindu wameshapatikana 100 wengine wameshakufa  jambo ambalo halina ukweli wala halijulikani limetokea wapi, Ili tuendelee kuilinda jamii ya Pemba juu ya majanga kama haya ya kipindu pindu  ambayo kwa zaidi ya miaka 6 hayajajitokeza ni nyinyi CHV kushirikiana na wanajamii kutoa elimu, kwa kushirikiana na waandishi wa habari". 

"Wao wanaelimisha kupitia vyombo vyao vya habari baada ya kupata usahihi kutoka wizara ya afya   na nyinyi mnaifikia jamii moja kwa moja kuwapa elimu ambazo mmepewa na wizara, juu ya mambo mbali mbali ikiwemo kutunza mazingira, kutumia chanjo, usafi na mambo mbali mbali ambayo yatasaidia 
 kupatikana kwa afya salama juu ya majanga mbali mbali kwa wananchi  ". 

Aidha wizara ya Afya mesema  kuwa mamlaka ya kutoa taarifa  endapo  nchi itapatwa  na  janga lolote   la maradhi mbali mbali  ni dhamana ya wizara hiyo hivyo  kusambaza uvumi ambao hautakuwa na  ukweli ndani yake  ni moja kati ya sababu ambazo hupelekea kuongeza taharuki na hofu kwa wananchi wenzao ambapo amewaasa watu wenye tabia hizo kuacha mara moja.

"Radio vifua mitaani huko  mara kumetokea  janga hili mara janga lile hizo tabia tuziwache mara moja za kuomba majanga, juu ya janga lolote litakalojitokeza wizara itawajuilisha wananchi kupitia waandishi wa vyombo mbali mbali, wala hatuombi kutokee majanga na ndio mana wizara haisinzii katika kuona wananchi wanakuwa salama tahadhari za kila aina zinachukuliwa".

Kwa upande wake mkuu wa kitengo cha  elimu ya afya Zanzibar Bakar Hamad Magarawa alisema kuwa lengo la kutolewa mafunzo hayo yaliyowashirikisha wanahabari na wahudumu wa afya jamii ni kusaidia kuongeza uelewa kwa wananchi juu ya kutofautisha uvumi na kujua usahihi wa taarifa mbali mbali za majanga. 

"Imekuwa ni desturi kila inapotokea janga uvumi unakuwa mwingi kuliko usahihi, lilipotokea janga la korona apa uvumi ulishika kasi hofu kwa wananchi zikajaa kiasi ambacho mtu anaogopa hata kukohoa, ili kuepusha hayo tumeona ipo haja kutoa elimu hii kwa vile  nyinyi ni watu ambao mnaaminika zaidi na jamii. "

Akizungumza  afisa mawasiliano magonjwa ya miripuko  kutoka  Shirika la Afya Duniani W. H. O. Julieth Rangi  amewaasa washiriki wa mafunzo hayo kuweka mikakati  maalum katika kuelimisha jamii juu ya magonjwa ya miripuko na majanga mbali mbali kwa kushirikiana na wizara hiyo ambapo shirika litaendelea kushirikiana katika kuiweka jamii iliyo  salama. 

Mafunzo hayo ya siku moja yamewashirikisha   Wahudumu wa Afya jamii  CHV, Wilaya ya Micheweni, Wete, Chake na Mkoani pamoja na waandishi wa radio za kijamii zilizopo kisiwani Pemba, Tv za mitandaoni, Pamoja na baadhi ya Vyombo vya habari vya Serikali kisiwani humo.

Mwisho 

Comments

Popular posts from this blog

BARABARA 19 KUJENGWA KWA KIWANGO CHA LAMI PEMBA KUKAMILIKA DISEMBA 2024.

WAZAZI ZIDISHENI KUFUATILIA NYENENDO ZA WATOTO HUSUSAN NI VIJANA .

UONGOZI WA WILAYA CHAKE CHAKE KFHI WAPONGEZA JUHUDI