Haya hapa Mazuri Yaliofanywa na Mkuu wa wilaya ya Magharib B Hamida Mussa Khamis Wananchi ,Wajivunia Mabadiliko katika ukuwaji wa Maendeleo nyanja Mbali mbali
NA ASIA MWALIM
"KUWA Mkuu wa wilaya ni jukumu kubwa na zaidi kwa wanawake, watu wengi hutupa changamoto kwa kuangalia jinsia zetu, lakini wanakuta tupo imara licha ya ujana jike wetu".
Hayo ni maneno ya kiongozi mwanamke ambae ni Mkuu wa Wilaya ya Magharibi B, Hamida Mussa Khamis(45 )aliebahatika kupata uteuzi wa nafasi hiyo kutoka kwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi.
Licha ya uongozi, mwanamke huyo ni mama wa familia yenye watoto watatu 3, 1 wakiume na 2 wakike na pia anapokua nyumbani kwake anapenda zaidi kupika.
Mwanamke huyo ni mfano wa kuigwa na wanawake wengine kwani ni miongoni mwa wanawake alietumika serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika awamu zilizopita na pia kuendela kupata nafasi nyengine ya uongozi katika awamu ya nane.
KABLA YA KUWA MKUU WA WILAYA YA MAGHARIBI B
Harakati za uongozi wa kuteuliwa kwa mwanamke huyo zilianza mwaka 2015, kupata nafasi ya Katibu Tawala wa wilaya ya Magharibi B, ambapo wakati huo mkuu wa wilaya hiyo alikua ni Ayoub Mohammed Mahmoud.
Anasema kwa mara ya kwanza alihisi ugumu kwa kua hakua mzoefu lakini kadri siku zilivyosonga mbele alizidi kuwa bora zaidi, na hilo ni kutokana na vitu alivyopewa kusimamia kwenda vizuri.
Alisema wakati huo alikua kiongozi mpya kwenye uteuzi lakini sio katika utendaji kwani alielekweza majukumu yake na alifanya wajibu wake vizuri katika miaka 2 ya ukatibu.
"Mwanamke hana ugeni, pia mama ni kiongozi, usemi huu ulikua akilini mwangu na kunipa ujasiri wa kufanya kazi vizuri kama ninavyoisimama majukumu ya familia yangu" alisema.
Nafasi nyengine alioitumika mwanamke huyo ni Katibu tawala Mkoa mjini Magharibi, kwa muda wa mwaka mmoja na miezi tisa katika mwaka 2017.
Alisema wakati huo, alijithidi kufuata miongozo anayotakiwa kufanya hasa miongozo ya serikali kuifanya kwa wakati kwani nafasi hiyo ni ya kiutendaji zaidi, pia iliongeza majukumu.
Katika uongozi wa awamu ya saba, chini ya Rais mstaafu, Dk.Ali Mohammed Shein alipata uteuzi wa kuwa mkuu wa wilaya ya kati, na kuhakikisha anatimiza wajibu wake kupitia sheria, sera na miongozo inayotolewa.
Amethibitisha kufanya kazi vizuri kumesaidia kupata nafasi ya kuongoza tena wilaya ya Magharibi B, baada ya kuonekana utendaji wake na juhudi zake zilizoonekana na serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar tangu awamu iliyopita.
TOFAUTI YA UONGOZI WAKE ULIOPITA NA SASA.
Takriban miaka miwili ameongoza wilaya hiyo ambayo amekiri ina ukubwa wa eneo, idadi ya watu na maendeleo pia ina mchanganyiko wa watu, ukilinganisha wilaya ya Kati.
Alisema miongoni mwa changamoto katika uongozi huo ni baadhi ya watu kukiuka sheria na kutofuata maelekezo ya serikali.
SIRI YA MAFANIKIO KATIKA UONGOZI WAKE.
Mara nyingi mwanamke mwenye malengo ya kufikia mbali katika uongozi, lazima atakua na kigezo, kinachompa ari, kwa upande wa bi hamida alipokua mdogo, alijifunza kupitia mwalimu wake bi khadija Bakari, na wakati huu jicho lake lipo kwa Mama samia ambae ni Rais wa Jamuhuri ya muungano waTanzania.
"Tunasimamiwa na kiongozi mwenye maono ya kuibadilisha Zanzibar sambamba na kuendana na kasi ya mabadiliko kwa kuzingatia mashirikiano, kutii maagizo kama wasaidizi wa Serikali, pia kupokea ushauri namna ya kuleta mabadiliko katika utendaji "
Kufanya vizuri kwenye nafasi anazopatiwa ni kutokana na elimu aliyoipata chuo cha uongozi na masuala ya ulinzi kwa mwaka 1, ambayo inatokana na juhudi za serikali kumpatia nafasi hiyo ili kumuandaa kuwa kiongozi bora.
Aidha aliipongeza serikali ya awamu ya saba chini ya uongozi wa Dk. Ali Mohammed Shein kwa kuona haja ya kumpatia elimu ya masuala ya uongozi ambayo imezaa matunda katika nchi hii.
Alisema alipokua mdogo aliongoza sehemu mbali mbali, kutokana na mazingira aliyopitia wakati akiwa mdogo, pia ni mkubwa katika familia yenye watoto 3 alisimama kama kiongozi kwa wenziwe.
Alisema kitu chengine kilichomjenga kutoa maamuzi wakati wowote ni mazingira aliyokulia kwani hakubahatika kuishi na wazazi wake bali alikua katika mazingira ya ulezini, na school bording huko moshi.
ALAMA NA KUMBUKUMBU NZURI KWA MUDA WA MIAKA 2 NDANI WILAYA HIYO.
Alifafanua kuwa changamoto haziwafanyi wanawake washindwe kutekeleza wajibu wao katika uongozi, na jamii inapaswa kuangalia uwezo wa wanawake na sio jinsia.
Miongoni mwa alama zisizo sahaulika katika uongozi wa awamu ya nane, kupitia mwanamke huyo ni kukubali kushuka kwa wananchi, na kusababisha wananchi wa maeneo mengi kukubaliana na harakati zake.
Jambo jengine alilofanikiwa Mwanamke huyo ni kusimamia ujenzi wa spitali ya wilaya katika eneo la Magogoni , pia usimamizi wa skuli ya Mama samia, ambayo imewakilisha vizuri suala la elimu katika wilaya hiyo.
Kitu chengine ni kutengeneza eneo maalumu la wajasirimali, ili kuweka pamoja wajasirimali, sambamba na kushirikiana na waekezaji mbali mbali ili kuanafanya waekezaji wawe huru na wafanye shughuli zao bila ya kuathiri sheria na tararibu za nchi.
AWAPA NENO WAZAZI ILI KUJENGA VIONGOZI WANAWAKE.
Kiongozi huyo alisema wazazi hawapaswi kuwalemaza watoto wa kike ambao wana nafasi ya kuwa viongozi bora wa baadae, badala yake kuweka usawa katika malezi yao.
"Kama wanawake wanoongoza wakati huu wasinge andaliwa mapema basi tusingelifikia kupata viongozi wanawake, tunao waona ukizingatia huu ni wakati wa sayansi na teknelojia" alisema.
Aliwashauri watoto wa kike wanaotamani kuwa viongozi watumie jitihada zaidi katika masomo kufikia ndoto zao, ili kujiletea maendeleo yao na taifa Lao, sambamba na kutokubali kukatishwa tamaa.
FAMILIA YA KIONGOZI HUYO
Wana familia ambao hawakuridhia majina yao yatajwe, ikiwemo mume wa kiongozi huyo, alisema mke wake ni mshauri wake mkubwa katika mambo mengi ya maendeleo.
Alisema yeye sio kiongozi lakini anatambua harakati za mkewe, na amejitolea kumpa ushirikiano katika hali yoyote bila ya kujali, kikubwa ni kuhakiksha anaitunza familia.
VIONGOZI WENGINE WA WILAYA HIYO.
Mkurugenzi wa Manispaa ya Magharibi B, Khadija Said Simai, alisema sio jambo rahisi analofanya mwanamke huyo, kuongoza bila hofu wilaya yenye ukubwa wa watu na majengo, anapaswa kupongezwa na kuigwa na wengine.
Alisema kiongozi huyo amepambwa na sifa nyingi wilayani humo, ikiwemo mashirikiano, mchapakazi, muajibikaji, na mara nyengine hufanya maamuzi magumu ya kuwashangaza wanaume.
WANANCHI.
Fatma Ramadhan Said, Safinia Issa Pamoja na Asha Abass ni wakaazi wa Wilaya hiyo, walisema hatua zilizofikiwa na Mwanamke huyo zimeanza kuleta mabadiliko ambayo yataboresha huduma za kijamii, kukuza maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi pamoja na kuondoa usumbufu wa kufata huduma bora nje ya wilaya hiyo.
KATIBA YA ZANZIBAR
Kwa mfano katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, katika kifungu 21(2) kila mzanzibari anayo haki na uhuru wa kushiriki kwa ukamilifu katika kufikia uamuzi juu ya mambo yanayomuhusu na yanayohusu taifa lake.
DIRA YA ZANZIBAR 2050
Aidha Dira ya Zanzibar katika maazimio ya 2.5.1 hadi 2.5.9 yameeleza masuala mbali mbali ya usawa wa jinsia na kuondoa unyanyasaji wa kijinsia pamoja na kuimarisha mifumo ya uwezeshaji wanawake ikiwemo kuinua na kutoa nafasi za uongozi kwa wanawake katika jamii.
Pia kuongeza fursa na kuwawezesha katika vyombo vya kutolea maamuzi na kwenye shughuli za uchumi, kijamii, siasa katika ngazi zote za utawala na huduma za sheria.
BAADHI YA MIKATABA INAVYOSISITIZA WANAWAKE KUONGOZA
Kwa mujibu wa Katiba Ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977,Ibara ya 5(1) mtu yeyote bila kujali jinsia (mwanaume au mwanamke) mwenye umri usiopungua miaka 18 ana haki ya kuchagua au kuchaguliwa kuwa kiongozi (Ibara ya 5(1)).
Comments
Post a Comment